ESCROW: Chenge akwaa kisiki.

21:30 by Kwetuhouse Media


Jitihada za Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), Andrew Chenge kutaka asihojiwe na Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma ‘zimekwaa kisiki’,  baada ya shauri la pingamizi lake alilofungua Mahakama Kuu kutupwa.

Chenge ni miongoni mwa watumishi wa Umma waliotajwa katika kashfa ya mgawo wa fedha za akaunti ya Tegeta Escrow zilizotolewa na mfanyabiashara maarufu nchini, James Rugemalira.

Februari 25, mwaka huu Chenge baada ya kusomewa mashtaka tisa na baraza hilo ya kudaiwa kuisababishia hasara Serikali,  kabla ya kuhojiwa aliwasilisha pingamizi la amri ya Mahakama linalodai kuzuia mamlaka zozote kujadili au kufanya kazi ya suala lolote la kashfa ya kampuni ya IPTL  ya uchotaji wa fedha kiasi cha Sh. bilioni 200 kwenye akaunti hiyo iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Siku iliyofuata  Baraza hilo chini ya Mwenyekiti, Jaji Mstaafu, Hamisi Msumi, lilitupilia mbali pingamizi hilo na kueleza kuwa lina haki ya kumhoji Chenge, lakini hakukubaliana na uamuzi huo na kusema anakata rufaa Mahakama Kuu kuomba mwongozo wa mahakama kuhusu kuendelea kujadiliwa suala hilo au la.

Katika kesi namba 18 ya mwaka 2015 ya Kikatiba iliyofunguliwa na Chenge Mahakama Kuu akidai haki yake ya kikatiba inakiukwa na kuiomba Mahakama kuzuia mashauri dhidi yake katika Baraza hilo yasiendelee.

Jana Jopo la Majaji wa mahakama hiyo jijini Dar es Salaam, Gadi Mjema, Fauthi Twaibu na Rose Teemba, walisikiliza mapingamizi yaliyowekwa na Chenge na washtakiwa Juni 1 na 2, mwaka huu.

Wakati wa maamuzi kulikuwa na Majaji wawili ambao ni Mjema na Twaibu, ambapo Jaji Twaibu akisoma uamuzi alisema baada ya kusikiliza pande zote Mahakama imeridhishwa na maelezo yaliyotokewa.

Alisema upande wa washtakiwa waliowekewa pingamizi walidai  mahakama haina mamlaka ya kuzuia kutohojiwa kwa mlalamikaji. Pia kwamba alikuwa na njia mbadala za kutatua kesi kabla ya kuifikisha mahakamani na alikuwa hana kesi ya msingi dhidi ya washtakiwa.

Jaji Twaibu alisema kesi imetupiliwa mbali na kwamba mapingamizi matatu ya washtakiwa yana msingi kwamba Baraza hilo lina uwezo wa kuendelea na shauri dhidi ya Chenge.

Akizungumza na NIPASHE Jumamosi jana kwa njia ya simu baada ya pingamizi lake kugonga mwamba, Chenge alisema anaamini ametendewa haki.

 “Nimetendewa haki, huo ndio uamuzi wa mahakama nimeridhika nao sina la kusema,” alisema Chenge huku akicheka.
Ofisa Habari wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Johanither Barongo, liliambia gazeti hili kuwa, wamepata taarifa dhidi ya maamuzi ya mahakama na kwamba watatoa taarifa zaidi Jumatatu.

Gazeti hili lilipomtafuta Jaji Msumi ili kujua lini watamuhoji Chenge, alisema  maamuzi yatatokana na tume.

CHANZO: NIPASHE


0 comments:

Post a Comment