Jitihada
za Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), Andrew Chenge kutaka asihojiwe na
Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma ‘zimekwaa kisiki’, baada ya
shauri la pingamizi lake alilofungua Mahakama Kuu kutupwa.
Chenge ni
miongoni mwa watumishi wa Umma waliotajwa katika kashfa ya mgawo wa fedha za
akaunti ya Tegeta Escrow zilizotolewa na mfanyabiashara maarufu nchini, James
Rugemalira.
Februari
25, mwaka huu Chenge baada ya kusomewa mashtaka tisa na baraza hilo ya kudaiwa
kuisababishia hasara Serikali, kabla ya kuhojiwa aliwasilisha pingamizi
la amri ya Mahakama linalodai kuzuia mamlaka zozote kujadili au kufanya kazi ya
suala lolote la kashfa ya kampuni ya IPTL ya uchotaji wa fedha kiasi cha
Sh. bilioni 200 kwenye akaunti hiyo iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
Siku
iliyofuata Baraza hilo chini ya Mwenyekiti, Jaji Mstaafu, Hamisi Msumi,
lilitupilia mbali pingamizi hilo na kueleza kuwa lina haki ya kumhoji Chenge,
lakini hakukubaliana na uamuzi huo na kusema anakata rufaa Mahakama Kuu kuomba
mwongozo wa mahakama kuhusu kuendelea kujadiliwa suala hilo au la.
Katika
kesi namba 18 ya mwaka 2015 ya Kikatiba iliyofunguliwa na Chenge Mahakama Kuu
akidai haki yake ya kikatiba inakiukwa na kuiomba Mahakama kuzuia mashauri
dhidi yake katika Baraza hilo yasiendelee.
Jana Jopo
la Majaji wa mahakama hiyo jijini Dar es Salaam, Gadi Mjema, Fauthi Twaibu na
Rose Teemba, walisikiliza mapingamizi yaliyowekwa na Chenge na washtakiwa Juni
1 na 2, mwaka huu.
Wakati wa
maamuzi kulikuwa na Majaji wawili ambao ni Mjema na Twaibu, ambapo Jaji Twaibu
akisoma uamuzi alisema baada ya kusikiliza pande zote Mahakama imeridhishwa na
maelezo yaliyotokewa.
Alisema
upande wa washtakiwa waliowekewa pingamizi walidai mahakama haina mamlaka
ya kuzuia kutohojiwa kwa mlalamikaji. Pia kwamba alikuwa na njia mbadala za
kutatua kesi kabla ya kuifikisha mahakamani na alikuwa hana kesi ya msingi
dhidi ya washtakiwa.
Jaji
Twaibu alisema kesi imetupiliwa mbali na kwamba mapingamizi matatu ya
washtakiwa yana msingi kwamba Baraza hilo lina uwezo wa kuendelea na shauri
dhidi ya Chenge.
Akizungumza
na NIPASHE Jumamosi jana kwa njia ya simu baada ya pingamizi lake kugonga
mwamba, Chenge alisema anaamini ametendewa haki.
“Nimetendewa
haki, huo ndio uamuzi wa mahakama nimeridhika nao sina la kusema,” alisema
Chenge huku akicheka.
Ofisa
Habari wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Johanither Barongo, liliambia
gazeti hili kuwa, wamepata taarifa dhidi ya maamuzi ya mahakama na kwamba watatoa
taarifa zaidi Jumatatu.
Gazeti
hili lilipomtafuta Jaji Msumi ili kujua lini watamuhoji Chenge, alisema
maamuzi yatatokana na tume.
CHANZO:
NIPASHE


0 comments:
Post a Comment